Meneja wa Liverpool Kenny Dalglish nae amejumuika na Klabu yake Liverpool na Mchezaji wao Luis Suarez kuomba radhi kuhusu kitendo cha fedheha cha Mchezaji huyo cha kukataa kupeana mkono na Patrice Evra kabla ya mechi ya jana Ligi Kuu England kati ya Manchester United na Liverpool kuanza Uwanjani Old Trafford na kwisha kwa Liverpool kubondwa bao 2-1.
Dalglish yeye ameomba radhi kuhusu mahojiano yake na Wanahabari mara baada ya mechi hiyo aliposema hakujua kama Suarez alikataa kumpa mkono Evra, ambacho ni kinyume na makubaliano yao yaawali klabuni, na kusisitiza kuwa Suarez hapaswi kulaumiwa kwa lolote lililotokea kwenye mechi hiyo.
Akiomba radhi Dalglish alitamka: ‘Nilipoongea jana kwenye TV sikuwa nimeona nini kilitokea lakini sikutenda kama apasavyo Meneja wa Liverpool katika mahojiano yale na naomba radhi kwa hilo.!’
Aliongeza: ‘Ian Ayre [Mkurugenzi Mtendaji wa Liverpool] ameshatoa msimamo wa Klabu na ni sahihi kwa Suarez kuomba radhi kwa nini kilichotokea Old Trafford. Kama alivyosema Ayre, sote tuna wajibu kuiwakilisha Klabu hii kwa njia bora na sahihi na hili linanihusu mie pia kama Meneja wa Liverpool.’
Hata hivyo kuna duru za Wadau zimesisitiza Dalglish alishindwa kuuzima mgogoro huu na badala yake kuuchochea kabla ya mechi ya Old Trafford pale alipodai Suarez hakupaswa kufungiwa kitu ambacho kilimfanya Sir Alex Ferguson wa Man United ashangae na kusema kama hiyo ilikuwa imani kwa nini hawakukata Rufaa baada ya Suarez kuadhibiwa kifungo cha mechi 8.