Straika wa Liverpool Luis Suarez ameomba radhi rasmi kwa kitendo chake cha kukataa kupeana mkono na Patrice Evra kabla ya mechi ya jana Ligi Kuu England kati ya Manchester United na Liverpool kuanza Uwanjani Old Trafford na kwisha kwa Liverpool kubondwa bao 2-1.
Tovuti ya Liverpool imetoa tamko la Suarez ambae amesema: ‘Nimeongea na Kenny Dalgish baada ya mechi na sasa nimegundua nimefanya makosa. Sikumwangusha yeye pekee bali Klabu yote na nini msimamo wake na naomba msamaha. Nimefanya kosa na najutia kwa kile kilichotokea.’
Aliongeza: ‘Nilipaswa kupeana mkono na Patrice Evra kabla ya mechi na naomba radhi kwa vitendo vyangu. Ningependa tuyaache haya yote nyuma na tugange yajayo na nitilie mkazo soka.’
Pia Mkurugenzi Mtendaji wa Liverpool, Ian Ayre, alitoa taarifa yake na kusikitishwa na kitendo cha Suarez ambae aliahidi kabla ya mechi atapeana mkono na Evra lakini hakufanya hivyo na hilo limeikera Klabu.
Ayre alisema: ‘Ni makosa kutudanganya na ni kosa kutompa mkono Evra. Amejiangusha yeye mwenyewe, pia amemwangusha Kenny Dalglish, Wachezaji wenzake na Klabu. Tumemwambia waziwazi matendo yake hayakubaliki Klabuni.’