Manchester City imeamua kutokata rufaa kupinga mashitaka dhidi ya ‘Toto Tundu’ wao Mario Balotelli aliyofunguliwa na FA baada ya kuonekana akimtimba kichwani Scott Parker wa Tottenham na hivyo atatumikia kifungo cha mechi 4 kinachoanzia mechi ya leo ya marudiano ya Nusu Fainali ya Carling dhidi ya Liverpool.
Mechi nyingine ambazo atazikosa Balotelli ni zile za Ligi Kuu England dhidi ya Everton, Fulham na Aston Villa.
Mashitaka ya Balotelli yalizuka kwa kitendo chake hicho kilichotokea kwenye mechi ya Ligi Kuu Jumapili iliyopita ambayo Man City walishinda 3-2 na bao la ushindi kufungwa na Balotelli katika dakika za majeruhi kwa penati.
Kawaida makosa kama ya Balotelli ni kifungo cha mechi 3 lakini kwa vile alishawahi kutolewa kwa Kadi Nyekundu Msimu huu katika mechi na Liverpool Mwezi Novemba kifungo huwa kinakuwa mechi 4.
Wakati Balotelli anaanza kifungo chake leo, Mchezaji mwingine wa Man City aliekuwa kwenye kifungo cha mechi 4, Vincent Kompany, ambae nae alipewa Kadi Nyekundu walipofungwa na Man United kwenye FA Cup, leo ndio anamalizia mechi yake ya mwisho ya kifungo chake ambacho pia Man City walinywea kukata rufaa aliposhitakiwa na walikubali adhabu ya mechi 4 kwa vile pia aliwahi kupewa Kadi Nyekundu mwanzoni mwa Msimu huu.

![]() |
Maoni