Mchezaji mwenye vituko na vitimbwi wa Manchester City Mario Balotelli amefunguliwa mashitaka na FA, Chama cha Soka England, kwa kumtimba kichwani Scott Parker kwenye mechi ya Ligi Kuu England iliyochezwa Jumapili Uwanjani Etihad na Man City kuishinda Tottenham bao 3-2.
Balotelli, alieingizwa Dakika ya 65 kwenye mechi hiyo, alipewa Kadi ya Njano na Refa Howard Webb kwa kumchezea faulo Benoit Assou-Ekotto lakini baadae alipomkanyaga Scott Parker Refa Webb hakuliona tukio hali na katika dakika za majeruhi, huku ngoma ikiwa 2-2, Balotelli aliifungia Man City bao la penati na kuwapa ushindi wa bao 3-2 na kujikita kileleni mwa Ligi wakiwa pointi 3 mbele ya Mabingwa Man United.
Akipatikana na hatia kwenye mashitaka yake haya Balotelli atafungiwa mechi 3 lakini kwa vile tayari Msimu huu alishatolewa nje kwa Kadi Nyekundu itabidi atumikie kifungo cha mechi 4.
Mchezaji huyo amepewa hadi Jumatano Saa 3 Usiku, saa za bongo, kujibu mashitaka hayo na akikiri makosa adhabu yake itaanza mara moja na ataanza kifungo chake kwa kuikosa mechi ya Jumatano ya marudiano ya Nusu Fainali ya Carling Cup na Liverpool itakayochezwa Anfield, ambayo Man City wanahitaji kuipiku Liverpool baada ya kufungwa bao 1-0 katika mechi ya kwanza, na mechi za Ligi dhidi ya Everton, Fulham na Aston Villa.
Lakini akikana mashitaka hayo Balotelli ataruhusiwa kucheza mechi na Liverpool Jumatano na kesi yake itasikilizwa kabla ya mwisho wa Wiki na akipatikana na hatia huenda akaadhibiwa zaidi ya kifungo cha mechi 4.

![]() |