Ripoti Spesheli

OLE GUNNAR SOLSKJAER=Sasa ni ‘Fergie wa Norway’

Ijumaa, 03 Februari 2012 07:17
Chapisha Toleo la kuchapisha

OLE_GUNNAR_SOLKSJAER_WITH_HIS_TEAM12Mara baada ya kuchapwa bao 5-0 na Haugesund Mwezi Mei, 2011, Ole Gunnar Solskjaer aliamua kuwapa hotuba Wachezaji wa Timu yake Molde ya huko Norway.

Aliwaambia: ‘Vijana, kama kuna chochote kilichobaki kwenu basi nitachukua pesa zenu zote, mikopo ya nyumba zenu na kuzichezea kamari kwamba tutachukua Ubingwa wa Ligi Msimu huu! Nadhani hili litatupa nafasi kubwa kushinda hiyo kamari!’

Solskjaer aliyajua maneno yote ya hotuba hiyo moyoni kwani aliyasikia zamani.OLE_GUNNAR_SOLSKJAER

Aliikariri hotuba hiyo yote Miaka 15 nyuma katika Msimu wake wa kwanza kama Mchezaji wa Manchester United pale Sir Alex Ferguson alipotoa spichi hiyo hiyo kwa Wachezaji wake wote kufuatia vipondo viwili mfululizo vya bao 5-0 toka kwa Newcastle na 6-3 toka kwa Southampton kwenye mechi za Ligi.

‘Naikumbuka Siku hiyo waziwazi!’ Solskjaer alisema huku akitabasamu. ‘Na kweli Msimu huo Man United walichukua Ubingwa kilaini!’

Na ndivyo walivyofanya Molde, chini ya Ole Gunnar Solskjaer alietua hapo Januari 2011, kwa kutwaa Ubingwa wao wa kwanza Nchini Norway tangu Klabu hiyo ianzishwe Miaka Miaka 100 iliyopita.

Ole Gunnar Solskjaer alianza kujiandaa kuwa Meneja tangu akiwa mdogo na kukazania zaidi akiwa Mchezaji.

Akiwa na Miaka 10 tu alikuwa akiwafundisha Watoto wenzake kucheza Soka Mtaani kwao huko Kristiansund, Norway.

Akiwa Man United alikuwa akiweka Kitabu cha Kumbukumbu yote yaliyokuwa yakitokea kwenye mazoezi, mechi na hata pale Nahodha Roy Keane akitukana au akimtukana wakati akikosa goli.

Lakini mwishowe Kitabu hicho cha Kumbukumbu kiligeuka kuwa kwa yale tu Sir Alex Ferguson aliyokuwa akiongea hasa mbinu, mikakati na tathmini ya Soka.

Solskjaer amebaini alipotua Molde aliigeuza Klabu hiyo kama Man United ndogo kutokana na ujuzi wake wa Miaka 15 wakati akiwa Manchester kwa kuiga kila kitu kuanzia mlo wa Wachezaji, uvaaji, na mazingira mengine yote aliyojifunza akiwa Old Trafford.

Alipostaafu kama Mchezaji wa Man United baada ya kuumia goti Solskjaer alipewa nafasi ya kuwa Meneja wa Timu ya Rizevu ya Man United na alipoamua kwenda Molde Solskjaer aliwachukua Makocha wasaidizi wa Man United, Mark Dempsey na Richard Hartis, ili kumpa sapoti.

Inadaiwa Ole Gunnar Solskjaer, ambae yupo kwenye historia iliyotukuka ya Man United kwa kuifungia bao la ushindi dakika za majeruhi kwenye Fainali ya UEFA CHAMPIONZ LIGI Mwaka 1999 walipowafunga Bayern Munich bao 2-1, yupo kwenye maandalizi kurudi Old Trafford kumrithi Sir Alex Ferguson akiamua kustaafu.
 

UCHAGUZI FIFA: Nani kumvaa Blatter?

Ijumaa, 11 Machi 2011 21:41
Chapisha Toleo la kuchapisha
SEPP_BLATTERKongresi ya FIFA itakutana tarehe 31 Mei 2011 na Juni 1, 2011 na moja ya ajenda yake ambayo ni nyeti mno ni uchaguzi wa Rais wa FIFA ambao kwa sasa unashikiliwa na Sepp Blatter, Raia wa Uswisi, tangu tarehe 8 Juni 1998 baada ya kumrithi Joao Havelange wa Brazil.
Tangu wakati huo, Blatter amekuwa akigombea tena na tena na kushinda vipindi vya uongozi wa Miaka minne wa FIFA wakati mwingine bila kupingwa.FIFA_LOGO
Tofauti na kura za kuchagua Uenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia ambazo Desemba 2010 zilizua utata mkubwa baada ya Urusi kushinda kuwa Mwenyeji wa 2018 na Qatar kwa Mwaka 2022 kwa madai kuwa ni kundi dogo tu la Watu 24 linafanya uteuzi huo, watu hao wakiwa ndio Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya FIFA, uchaguzi wa Rais wa FIFA hufanywa na Nchi Wanachama wote na kila Nchi ina kura moja na zipo Nchi wanachama 208.
Ingawa hadi sasa hakuna aliejitokeza kuwania nafasi hiyo ya Urais wa FIFA mbali ya Sepp Blatter kutangaza kitambo kuwa atagombea tena Urais kwa vile hajikamilisha majukumu na malengo yake kuna minong'ono Rais wa Shirikisho la Vyama vya Soka Barani Asia, AFC, Mohamed bin Hammam, Raia wa Qatar, huenda akajimwaga kwenye kinyang'anyiro hicho.
Kwa wadau wengi Blatter bado ndio mwenye nguvu na sapoti kubwa kutoka Nchi Wanachama hasa Afrika, wenye Wanachama 53 na hivyo kura 53 na huko Nchi za Carribean, Marekani ya Kati na Kaskazini, wenye kura 45, na Marekani ya Kusini, ambako zipo 10.
Asia wana kura 46.
Ulaya, wenye kura 53, wanaongozwa na Rais wao Michel Platini ambae inadaiwa ni sapota wa Blatter kwa vile tu wana makubaliano na Blatter, mwenye umri wa Miaka 73, kuwa hatagombea uchaguzi unaofuata Mwaka 2015 na atamwachia Platini mikoba yote.
Mbali ya Platini, Blatter anasapotiwa kwa karibu na Viongozi wa CAF, Issa Hayatou, na Jack Warner wa CONCAF, amblo ni Shirikisho la Nchi Wanachama kutoka Nchi za Carribean, Marekani ya Kati na Kaskazini.
 
 

RYAN GIGGS: Jumanne Machi 2 anatimiza Miaka 20 kuichezea Man United

Jumanne, 01 Machi 2011 22:20
Chapisha Toleo la kuchapisha

GIGGS11Bado yupo dimbani akiwa na umri wa Miaka 37 na hadi leo hii wapinzani wake wengi uwanjani wanashindwa kumkaba.

Ryan Giggs alianza kuivaa jezi ya Timu ya kwanza ya Manchester United tarehe 2 Machi 1991 Uwanjani Old Trafford alipoingizwa kuchukua nafasi ya Dennis Irwin katika mechi na Everton wakati huo akiwa na umri wa Miaka 17 tu.

Siku hiyo, Giggs alivaa jezi iliyoonekana kuwa kubwa kwake kwa umbo lake dogo na siku hiyo hapendi kuikumbuka kwani Man United walichapwa 2-0 na Everton.

Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United, amenena: “Miaka 20 ya kupanda na kushuka kwenye Winga ya kushoto!”

Giggs ana rekodi ya kipekee.

Amecheza kila Msimu tangu Ligi Kuu ianzishwe Mwaka 1991, kufunga goli kila Msimu wa Ligi Kuu tangu ianzishwe, ameshinda Ubingwa wa Ligi mara nyingi kupita Mchezaji yeyote na anashikilia rekodi ya kucheza mechi nyingi kwa Manchester United kupita Mchezaji yeyote katika historia ya Klabu hiyo.GIGGS12

Ikiwa Giggs atavaa jezi Man United wakicheza na Chelsea Jumanne usiku kwenye mechi ya Ligi Kuu huko Stamford Bridge atakuwa amefikisha mechi 606 za Ligi na hivyo kuifikia rekodi ya Sir Bobby Charlton ya kuwa Mchezaji wa Man United aliecheza mechi nyingi za Ligi kwa Manchester United.

Giggs aliivunja rekodi ya Sir Bobby Charlton ya kucheza mechi nyingi kwa Manchester United ambayo Charlton alikuwa akiishikilia kwa kucheza mechi 758 siku ile ya Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI huko Moscow, Urusi Mwaka 2008 Man United walipowatwanga Chelsea na kuchukua Ubingwa wa Ulaya.

Hadi leo Giggs amefikisha jumla ya mechi 861.

Katika Miaka yake 20 na Manchester United, Giggs amecheza kwenye Timu moja na Wachezaji 131 lakini moyoni anaamini Paul Scholes, Bryan Robson na Roy Keane ndio walikuwa bora.

Giggs anatamka: “Wakati ukicheza pamoja na Bryan Robson unaamini hamfungiki, Keane nae ilikuwa hivyo!”

HISTORIA YAKE KWA TAKWIMU:

-Kadi Nyekundu: 0

-Tuzo ya Goli la Msimu: mara 1 kwa goli lake lililoiua Arsenal Nusu Fainali ya FA Cup Mwaka 1999

-Tuzo ya Mchezaji Bora toka kwa PFA [Chama cha Wachezaji wa Kulipwa]: mara 1 Msimu wa 2008/9

-OBE, Tuzo toka kwa Malkia wa Uingereza, kwa utumishi uliotukuka kwenye Soka

-Digrii ya Sanaa ya heshima toka Chuo Kikuu cha Salford cha Manchester

-Ubingwa wa Klabu za Ulaya, Miaka ya 1999 & 2008

-Tuzo ya PFA ya Mchezaji Chipukizi: mara 1

-Tuzo ya BBC ya Mwanamichezo wa Mwaka: mara 3

-FA Cup: mara 4 Miaka ya 1994, 1996, 1999, 2004

-Kombe la Ligi [sasa Carling]: mara 4 Miaka ya 1992, 2006, 2009, 2010

-Kuwemo kwenye Timu Bora ya Msimu ya PFA: mara 9

-Ubingwa wa Ligi: mara 11 [HII NI REKODI PEKEE]

-Kucheza na Kufunga mfululizo kwenye Misimu ya UEFA CHAMPIONS LIGI: mara 11 [HII NI REKODI]

-Magoli kwa Timu ya Taifa ya Wales: 12

-Misimu 19 ya Ligi Kuu na kufunga mabao kila Msimu: Misimu 19 [NI REKODI NA YEYE NI MCHEZAJI PEKEE KUFANYA HILO]

-Ni Mtu wa 22 kupata Tuzo ya Mji wa Salford ya kuwa Mtu huru Jijini hapo

-Mara 64 amechezea Wales

-Magoli 158 ameifungia Manchester United

-Amecheze mechi 605 za Ligi kwa Manchester United [Mechi moja nyuma ya kuifikia rekodi ya Sir Bobby Charlton]  

-Amecheza Jumla ya Mechi 862 kwa Manchester United [HII NI REKODI KWA KUWA MCHEZAJI PEKEE ALIECHEZA MECHI NYINGI KATIKA HISTORIA YA KLABU HIYO]

 

UKAME wa MAKOMBE: Kilio Emirates, Carling Cup yawaponyoka!

Jumatatu, 28 Februari 2011 22:28
Chapisha Toleo la kuchapisha

MARTINS_ASHANGILIAMara baada ya kipenga cha mwisho cha Fainali ya Kombe la Carling Wachezaji wa Arsenal walisimama, walikaa chini au kupiga magoti Uwanjani Wembley wakiwa wamevunjika moyo kabisa.

Walitulia tuli kwa majonzi na walionekana kukata tamaa na nyuso za majonzi kama zile ambazo ulimwengu ulizishuhudia Mwaka 1999 wakati Bayern Munich waliponyukwa 2-1 na Manchester United dakika za majeruhi kwenye Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI Uwanjani Nou Camp.

Bao la dakika ya 89 la Straika kutoka Nigeria Obafemi Martins baada ya kujichanganya na kujikoroga kwa Kipa wa Arsenal Wojciech Szczesny na Sentahafu wake Laurent Koscielny kumeendeleza ukame wa Makombe huko Emirates ambao ulianza 2005.

Wengi waliamini Arsenal watashinda mechi hii lakini upiganaji na kujituma kwa Wachezaji wa Birmingham kuliwafanya waweze kuimudu Arsenal ambao kawaida ni watalaam wa kumiliki mpira, pasi za uhakika na mashambulizi mfululizo.

Uwanjani Wembley, Arsenal walionekana wasiotulia na wenye wasiwasi mkubwa pengine ulioletwa na matumaini makubwa ya kutwaa Kombe lao la kwanza baada ya muda mrefu.

Arsenal walianza mechi hii kwa bahati kubwa kufuatia uzembe wa Waamuzi.

Dakika mbili tu tangu gemu ianze gonga za Birmingham zilizoanza kwa Keith Fahey kwenda kwa Nikola Zigiz aliempenyezea Lee Bowyer aliechomoka na kuangushwa na Kipa wa Arsenal Wojciech Szczesny ziliinua Watu wengi waliotegemea penati na Kadi Nyekundu kwa Kipa wa Arsenal Wojciech Szczesny.MARTINS_ASHANGILIA2

Kwa mshangao uamuzi ulikuwa ni wa makosa kwamba Bowyer alikuwa ofsaidi.

Hata hivyo Birmingham hawakuvunjika moyo na wakafanikiwa kupata bao la kwanza mfungaji akiwa pande la mtu Nikola Zigic.

Nahodha wa Arsenal Robin Persie alisawazisha kwa bao tamu lakini wakati anafunga aliumia goti na baadae alishindwa kuendelea na Fainali hiyo na yupo kwenye hatihati kama atacheza mechi ya marudio na FC Barcelona huko Nou camp wiki ijayo.  

Bosi wa Arsenal, Arsene Wenger, yupo kwenye mtihani mkubwa wa kuipa upya Timu yake morali ili iendelee kupigana katika vinyang’anyiro walivyobaki kuwemo ambavyo ni Mataji matatu.

Kwenye Ligi Kuu bado wako kwenye picha wakiwa nafasi ya pili nyuma ya vinara Manchester United na wako pointi 4 nyuma yao huku zikiwa zimebaki mechi 11.

Jumatano Arsenal wapo Emirates kurudiana na Timu ndogo Leyton Orient kwenye Kombe la FA baada ya kutoka nao sare 1-1 na mshindi ataikwaa Man United kwenye Robo Fainali huko Old Trafford Machi 12.

Wiki inayokuja Arsenal wanatua Nou Camp kurudiana na FC Barcelona kwenye UEFA CHAMPIONS LIGI baada ya kuwatwanga 2-1 Uwanjani Emirates wiki mbili zilizopita.

Huku wakikabiliwa na mitihani hiyo, Wenger amejaribu kuwaliwaza Wachezaji wake: “Inavunja moyo sana lakini tuna changamoto kubwa mbele yetu. Carling Cup ni mechi 4 au 5 lakini Ubingwa wa Ligi ni mechi 38 hivyo hatuwezi kutupa mechi 38 kwa kufungwa gemu moja tu! Nina imani tuna moyo wa kijasiri na hii ni nafasi yetu kudhihirisha hilo! Tutaulizwa maswali mengi kuhusu makosa yetu lakini lazima tuwe imara kukabiliana na hali hii.”

Wenger amekiri Koscielny na Szczesny wameathirika mno na makosa yao Uwanjani Wembley.

Wenger amesema: “Wote wamefadhaika mno. Lazima tuwapoze na kuwasaidia. Ni wajibu wa Timu kusaidiana. Lilikuwa kosa la kutokuwa na mawasiliano na mpira ukitua kwenye utata siku zote ni lazima uondoe kabisa na si kusita!”

 

OLD TRAFFORD: Nyumba Hii Haiuzwi!!

Jumamosi, 26 Februari 2011 13:33
Chapisha Toleo la kuchapisha

OLD_TRAFFORDbestWamiliki wa Manchester United, Familia ya Kimarekani ya kina Glazer, imekanusha na kukataa kuwa wako mbioni kuiuza Klabu hiyo na msistizo huo ulitolewa wakati Wamiliki hao wakitangaza Mahesabu ya Klabu ya Nusu Mwaka ya Mwaka wa Kifedha.

Hivi karibuni kumekuwa na uvumi kuwa Qatar ipo mbioni kuinunua Man United lakini pande zote mbili zimekanusha uvumi huo.

Manchester United imetangaza kuwa Mapato yao, kabla ya Riba, Kodi na kushuka thamani kwa mali zao, yameongezeka kwa Asilimia 3.2 na kufikia Pauni Milioni 60.6 kwa Miezi 6 iliyoishia Desemba 2010 na makusanyo yao yameongezeka kwa Asilimia 8.2 na kufikia Pauni Milioni 156.5.

Msimu uliokwisha Manchester United ilikumbwa na upinzani mkubwaLOVE_UNITED12 kutoka kwa Washabiki ambao waliendesha upinzani kuipinga Familia ya Glazer huku wakivaa Rangi za Kijani na Dhahabu ambazo ni rangi za Klabu ya Newton Heath iliyoanzishwa mwaka 1878 na hapo tarehe 26 Aprili 1902 kubadilishwa jina kuitwa Manchester United ambao walianza kutumia Jezi za rangi Nyekundu, Nyeusi na Nyeupe.

Wakati Mashabiki hao wakiendesha kampeni hiyo ya upinzani nje na ndani ya Old Trafford wakati huo kukazuka Kikundi cha matajiri kilichojiita ‘Red Knights’ waliotaka kukusanya nguvu kifedha kuinunua Man United lakini kina Glazer walisimama kidete kugomea ofa zao.

Red Knight wakasalimu amri na kukiri kushindwa kuitwaa Man United toka kwa kina Glazer.

Familia ya Glazer iliinunua Man United Mwaka 2005.

TIJUKUMBUSHE:

MAKALA==Jumamosi, Februari 10, 2010 kutoka Blogu www.uksokainbongo.blogspot.com

Washabiki Man United wapinga kina Glazer!!!

• Wavaa Kijani na Dhahabu ishara ya upinzani!!

Hivi karibuni katika kila mechi ya Manchester United, rangi za kijani na dhahabu zimekuwa zikionekana miongoni mwa Washabiki wa Klabu hiyo na hizi ni rangi za Klabu ya Newton Heath iliyoanzishwa mwaka 1878 na hapo tarehe 26 Aprili 1902 kubadilishwa jina kuitwa Manchester United na rangi kuwa nyekundu, nyeusi na nyeupe.

Newton Heath ilianzishwa na Wafanyakazi wa Depo iliyokuwepo Newton Heath la Reli ya Lancashire na Yorkshire..

Mwaka 2005 Familia ya Matajiri kutoka Florida Marekani iitwayo Glazer iliinunua Manchester United na kuiingiza kwenye deni kubwa ambalo, ingawa Menejimenti ya Klabu inadai hilo deni ni kitu cha kawaida na uwezo wa kulilipa upo, Washabiki hawapendeziwi nalo na wameanzisha upinzani mkubwa kwa Familia ya Glazer.

Ndio maana Mashabiki, kwenye mechi za Manchester United, wanavaa skafu, fulana na kofia rangi za kijani na dhahabu ikiwa ni alama ya chimbuko la Manchester United, Klabu ya Newton Heath iliyoanzishwa na Wafanyakazi makabwela wa Depo ya Reli.

Nje ya Uwanja wa Old Trafford fulana za rangi hiyo ya kijani na dhahabu huuzwa huku nyuma zina maandishi [Shairi la Kiingereza] na tafsiri ya haraka ni:

GREEN_N_GOLDRoho ya United haiuzwi, Ndio maana kwa fahari tunavaa Kijani na Dhahabu,

Hatutavaa ile Jezi Nyekundu inayosifika, Mpaka Glazer waondoke au wafe,

Hivyo inua viwango vya zamani juu, Kwa Kijani na Dhahabu tutaishi na kufa,

Na hakika siku itafika tena, Tutakapovaa Nyekundu yetu kwa mara nyingine tena!”

Upinzani huu wa Washabiki umepamba moto na sasa kuna habari kwamba kuna Kikundi cha Matajiri ambao ni Mashabiki wa Manchester United wameanzisha umoja ili kuing’oa Klabu hiyo mikononi mwa Familia ya Glazer.

Matajiri hao wanafanya mikakati na kukusanya uwezo ili kuinunua Klabu hiyo.

Nae Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United, akizungumzia sakata hilo la Mashabiki amesema anaelewa uchungu wa Mashabiki ingawa amekiri wale walio madarakani wanafanya kila lililo sahihi kwa maendeleo ya Klabu hiyo.

Inasemekana Mashabiki wanajikusanya ili kufanya maandamano huku kila mtu akivaa kijani na dhahabu kabla ya mechi ya Machi 10 ya marudiano ya UEFA CHAMPIONS LIGI na AC Milan Uwanjani Old Trafford.

Ferguson amesema: “Hilo halinihusu. Hatujali wanavaa rangi gani kwani wote bado wanaisapoti Timu moja tu! Hili linaonyesha

Mashabiki wana uchungu na Timu yao!”

Ferguson ameongeza: “Kila Shabiki ana haki ya kulalamika kwa kile wanachoona ni haki lakini inabidi na sie tuiendeshe Klabu kwa njia sahihi. Misingi ya Klabu hii bado ni mizuri! Tuna Timu ya Vijana nzuri na Timu ya kwanza inafanya vizuri sana! Sisi tunaendelea na upande wa soka na wao waendelee tu mradi hawaathiri Timu.”

 


Ingia

Jiandikishe / Ingia

adidas

All Originals 300x250

MATANGAZO

Adidas Predator 300x250

TANGAZA HAPA

All Originals 728x90