Kanisa kulishitaki Vuvuzela Afrika Kusini
Habari zitokazo huko Kwa-Shangase, Kwa Zulu-Natal, zimesema kuna Madhehebu ya kale huko Afrika Kusini yaitwayo Kanisa la Kibaptisti ya Nazareth, jina la kiasili ni ‘Shembe’, yamo njiani kufungua kesi Mahakamani kupinga matumizi ya ‘Vuvuzela’ kwenye Viwanja vya Soka na hasa kwenye Fainali za Kombe la Dunia zitakazochezwa Afrika Kusini kuanzia Juni 11 hadi Julai 11.
Msemaji wa Shembe, Enoch Mthembu, anadai Vuvuzela ni mali ya Kanisa lao na limeibiwa na Washabiki wa Soka na wameahidi kufungua kesi Mahakamani kupinga matumizi yake mipirani.
Shembe hulitumia Vuvuzela katika Mtembezi yao makubwa ya kila mwaka wakizifuata nyayo za Mwanzilishi wa Kanisa lao Isaiah Shembe alipotembea kwenda Mlima Mtakatifu wa Nhlangakazi huko Kaskazini ya Mji wa Durban, Kwa Zulu-Natal mwaka 1910.
Matembezi hayo matakatifu ambayo kila mwaka huwa na Wafuasi zaidi ya 300,000 huandamana na milio ya Vuvuzela.
Shembe wanadai kuna Shabiki mmoja wa Kaizer Chiefs, ambayo ndiyo Klabu kubwa Afrika Kusini, alilitembelea Kanisa lao kwenye miaka ya mwanzoni 1990 na ‘kuiba’ hilo Vuvuzela.
Vuvuzela limevuta hisia nyingi katika ulimwengu wa Soka huku baadhi ya Nchi zikitaka lipigwe marufuku kwenye Fainali za Kombe la Dunia kwa kuwa na kelele nyingi na kusumbua Wachezaji, Watazamaji na Makampuni yanayopeperusha matangazo ya moja kwa moja ya TV.
Hata hivyo FIFA imesema Vuvuzela litaendelea kwa sababu ni utamaduni wa Soka ya Afrika Kusini.