♦MECHI KUANZA SAA 12 JIONI KUPISHA MAZOEZI YA TWIGA STARS
Mabingwa wa Tanzania Bara Yanga leo wanajimwaga Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam kuikwaa JKT Ruvu katika mechi ya Ligi.
Mechi nyingine ambazo zitachezwa leo ni Ruvu Shooting v Kagera Sugar huko Mlandizi, Pwani na Villa Squad v Toto African huko Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.
Yanga wanaingia kwenye mechi ya leo wakiwa nafasi ya pili na wana pointi 28 huku Simba wakiongoza Ligi hiyo wakiwa na pointi 31.
JKT Ruvu wapo nafasi ya 8 wakiwa na pointi 16 na katika mechi yao ya mwisho ya Ligi walifungwa bao 1-0 na Polisi Dodoma.
Kwenye mechi yao ya mwisho, Yanga walitoka sare 2-2 na Moro United.
Kwa mujibu wa TFF, mechi hii ya Yanga itaanza Saa 12 Jioni badala ya Saa 10 na Nusu ili kuipisha Timu ya Taifa ya Wanawake, Twiga Stars, kufanya mazoezi yake kwa maandalizi ya mechi yao ya marudiano na Namibia itakayochezwa Uwanja wa Taifa Jumapili.
Mechi hiyo ya Twiga Stars pia imesababisha mechi ya Ligi Kuu kati ya Azam FC na Moro United iliyokuwa ichezwe Uwanja wa Chamazi Siku ya Jumapili isogezwe mbele hadi Jumatatu ili kuwapisha Mashabiki kushuka Uwanja wa Taifa kuishangilia Twiga Stars.
